Welcome to the blog of Mr. Chesco Kilemile who is a renowned singer who came on in the industry singing gospel music. If you like this blog tourism will get to know my work and events relating to the preparation of my work in general ..... thank you for visiting this blog .....

Sunday, September 20, 2015

Changamoto wanazozipata Watoto wanaohitimu Elimu ya Msingi bila kuchaguliwa Sekondari nchini

LENGO mojawapo la Elimu ya Msingi Tanzania ni kumuandaa mtoto aweze kuingia hatua ya pili ya elimu yaani Sekondari na Elimu ya Ufundi lakini pia kumwandaa mtoto kuingia  katika ulimwengu wa kazi na ajira.
Nikitafakari kwa makini naona ni wazi kuwa lengo hili halifikiwi  kwani watoto wengi wanaomaliza elimu ya msingi hawapati nafasi ya kuendelea na masomo ya sekondari au mafunzo  ya  ufundi na badala yake hurudi kijijini/mitaani na kuwa wanakijiji/wa mtaani.
Baadhi ya watoto hawa huwa hawajui kusoma na kuandika kutokana na hali halisi ya mfumo wa elimu ya Tanzania ulivyokaa na hawapati elimu ya uraia itakayowasaidia endapo hawataendelea na masomo. Elimu waipatayo inawaandaa kufaulu mtihani ili kuendelea na masomo na huwapa mwanga kidogo sana wa kuzikabili changamoto za maisha wale  ambao hawapati  fursa ya kuendelea na masomo.  
                                               
Watoto hawa wanaofeli  mtihani bado ni wadogo na mfumo wa elimu ya msingi hauwaruhusu tena kurudi shuleni ili kurudia masomo  yao, Wengi wa watoto hawa hutoka familia maskini zenye vipato vya chini  hivyo huwawia vigumu kujiunga shule  za binafsi na kama ikitokea ni kwa wachache ambao wazazi wao ama ni watumishi ama wafanya biashara wenye kipato kinachoeleweka. 
Kama nilivyosema hapo mwanzo, watoto hawa hupata elimu inayowaandaa kufaulu mtihani wa mwisho wa Darasa la Saba ili kuendelea na masomo ya sekondari kwahiyo watakao faulu, elimu itakuwa imewanufaisha lakini wale wasiobahatika elimu inakuwa haijawasaidia na watarudi nyumbani kuishi na wazazi wao katika hali zao za umaskini. 
Kumbuka kuwa hakuna elimu ya ujasiliamali inayofundishwa ili kuwandaa watoto hawa kuwa wajasiriamali, au elimu ya uraia itakayowaandaa kukabiliana na changamoto za maisha pindi warudipo nyumbani, wala hakuna chochote wanachokuwa wameandaliwa watakapofeli mtihani kwamba wanaweza kukifanya ili kujimudu kimaisha, wanakuwa hawana mtaji wa namna yoyote ile; si maarifa wala fedha.
Watoto hawa hupelekwa shuleni kutimiza wajibu kwa vile elimu ya msingi ni ya lazima kwa kila mtoto lakini hakuna anachoenda kukivuna zaidi ya kufikiria kufaulu mtihani kwenda sekondari na hali hii huendelea kuchangia umaskini kwa kiasi kikubwa nchini mwetu.
Watoto hawa hupatwa na madhara makubwa sana wasiostahili kuyapata, madhara yanayopelekea kujiingiza katika mitandao ya ajabu na michafu isiyofaa na kukubalika katika jamii zao ikiwemo utumiaji wa madawa ya kulevya, ulevi wakupindukia na uvutaji sigara, umalaya/ubakaji/ushoga/ukahaba,  wizi/ukabaji/ujangili na matendo mengine kama hayo yanayosababisha mifarakano kwenye familia na jamii kwa ujumla. 
Hali hii hutokea pale wazazi wanapoona kuendelea kuishi na watoto hao ni mzigo na hawawezi kuwahudumia hivyo watoto kukosa mahitaji yao ya msingi kutoka kwa wazazi wao. Hapo ndipo watoto hujiingiza katika ajira zisizo rasmi pia ndoa za utotoni zinazo sababisha mimba za utotoni na kupelekea zaidi umaskini  na ongezeko la magonjwa ya zinaa ikiwemo VVU/UKIMWI.
Watoto wengine huamua kujishughulisha na shughuli zingine za kiuchumi kama vile ukataji wa miti kwa ajili ya kuchoma mkaa na kupata kuni ili kuuza, uvuvi haramu wa kutumia sumu na zana zisizokubalika ili kujipatia kipato kwa haraka, uwindaji haramu wa wanyama pori mambo ambayo kwa pamoja huchangia uharibifu wa mazingira na ujangili. 
Wengine hujishughulisha na utengenezaji wa pombe haramu aina ya gongo na uuzaji wa madawa ya kulevya vinavyosababisha wao wenyewe kuwa watumiaji  na waathirika wakubwa. Watoto wengine huamua kuwa ombaomba na kuishia mitaani na kusababisha ongezeko la watoto wa mitaani.
Kwa changamoto hizi ni vigumu kwa Tanzania kuondokana na umaskini kama elimu ya msingi haitatazamwa na kufanyiwa marekebisho upya. Ikumbukwe kuwa  umri wa watoto hawa ni mdogo ambao ni kati ya miaka kumi na mbili na kumi na nne na hutambuliwa na sheria  kuwa ni  watoto lakini wanapohitimu na kutochaguliwa kuendelea na masomo husahaulika na kuachwa bila msaada wowote kutoka kwa wadau  wa elimu na  Serikali kwa ujumla. 
Hapo ndipo huamua kutafuta ajira na mara nyingi hujikuta wamejiingiza kwenye ajira hatarishi kwao kama vile kazi ngumu za mashambani, viwandani, migodini, na majumbani. Wakati mwingine sheria huwabana waajiri wa watoto hawa kuwa umri wao hauruhusu kutumikishwa na hapo ndipo najiuliza maswali haya:  je, watoto hawa watajikimu vipi ili hali hawana namna nyingine ya kutafuta kipato?
Kwa utaratibu huu tunawezaje kupunguza tatizo la watoto wa mitaani? Tatizo la mimba za utotoni litadhibitiwa vipi?, na tutawezaje kupunguza swala zima la ukabaji na wizi unaopelekea watoto hawa kubandikwa majina mabaya ya vibaka na  kuuwawa kikatili na pengine kwa kuchomwa moto?
Serikali na wadau wengine wote wa elimu wasipoliangalia swala hili kwa makini na kulitafutia ufumbuzi, itakuwa ni vigumu sana kuondokana na umaskini na  kuufuta ujinga utakaotokana na kushindwa kwa watoto hawa wanaogeuka kuwa wazazi wa umri mdogo kuwahudumia na kuwapa haki za msingi watoto wao wanaowazaa  kama vile elimu, chakula, mavazi, malazi, huduma za afya n.k  kutokana na kuwa na hali duni ya maisha wao na familia zao na hali hii itakuwa inajirudia mwaka hadi mwaka. 
Ushauri wangu kwa Serikali na wadau wote wa elimu yakiwemo mashirika yanayojishughulisha na watoto  wautazame upya mfumo huu wa elimu ya msingi ili ama watoto hawa wapewe fursa nyingine ya kurudi shuleni kusoma au waangalie uwezekano wa kutoa elimu maalumu kwa hawa watoto itakayowawezesha kujiandaa kukabiliana na changamoto wanazoenda kukutana nazo pindi warudipo uraiani.
Hii itawasaidia kupata fursa ya kujitegemea kiuchumi na kuondokana na utegemezi na umaskini ambao naamini chimbuko lake lipo hapa, hali itakayopelekea kukubalika katika familia zao na jamii kwa ujumla.
Sheria ya mtoto iliyowekwa iwabane wadau na Serikali kwa kuwatelekeza watoto hawa ambao umri wao ni chini ya miaka kumi na nane na kupambana na changamoto ambazo bado ni adhabu isiyowastahili kuipata na ninaamini ni haki ya msingi ya mtoto huyu wa maskini kuendelea kupata elimu hadi hapo atakapofikia umri wa utu uzima.

No comments:

Post a Comment